|
|
 |
ASILI YA KABILA NA UTARATIBU WA JAMAA
Utaratibu wa kabila la
Gikuyu wategemea mambo matatu makubwa, ambayo bila kuwako
hakuwezi kuwa na umoja katika shughuli za kabila. Kwani
tabia na hali ya kila mtu katika kabila la Gikuyu
hudhihirishwa na kanuni tatu kuu ambazo tutazieleza hapa kila moja.
Ya kwanza ni ujamaa
(mbari au nyumba) ambayo huunganisha watu wote wenye udugu wa damu; yaani
mwanamume, mkewe au wake zake na watoto na pia wajukuu wao, vitukuu na vilembwe.
Ya pili ni ukoo
(muhiriga) unaounga katika kundi moja vikundi vidogo vidogo vya mbari
ambavyo jina la ukoo wao ni moja na wanasadikiwa walitoka kwa jamaa moja zamani
za kale. Ni wazi kwamba kwa ajili ya desturi ya kuoa wanawake
wengi, jamaa moja au mbari huongezeka haraka, na katika kizazi kimoja
inawezekana mbari hiyo kuwa na watu mia moja au
zaidi. Kwa hivyo mnamo vizazi vichache idadi hiyo
huongezeka kuwa maelfu kadha, na hapo huwa shida kwa mbari hiyo
kuishi pamoja kama kundi moja ambako wangeitana baba,
mama, dada, ndugu, mjomba, shangazi, babu, nyanya na
kadhalika.
Vitambulisho hivi vya
udugu wa damu vikitoweka, kiungo cha pekee kinachobaki katika kundi ambalo hapo
zamani lilikuwa limeunganishwa na uhusiano wa damu ya karibu karibu, ni
muhiriga tu. Muhiriga hufunga-manisha pamoja jamaa wasiokaribiana
na hii huwafanya wafikirie kusaidia-na katika mambo yote muhimu kwa manufaa na
starehe ya muhiriga. Ili wazo hili lisisahauliwe, watu wa muhiriga
mmoja hukutanika kwa kawaida wakati wa sherehe kubwa
kubwa, vile kama arusi na tohara. Katika sherehe hizo wazee wa
kila mbari humleta kijana mmoja. Vijana hawa huletwa pamoja
wakajulishwa kila mmoja kwa mwenzake na kuelezwa vile
ukoo wao unavyounga mbari yao kwa muhiriga. Vijana
hao huelezwa mambo haya ili kwamba wakiwa watu wazima na
kuchukua madaraka katika uongozi wa mbari zao, waweze kuendesha
kwa busara shughuli za jamaa zao, na kadhalika wafuate
mwenendo mzuri kama babu zao katika kukuza umoja wa
muhiriga mzima.
Kanuni ya tatu kubwa
katika kufanya Gikuyu kuwa kitu |kimoja ni desturi ya hirimu (riika).
Kama tulivyoona, utaratibu wa mbari na muhiriga husaidia kuunda makundi
ya jamaa ndani ya kabila; kila kikundi kikiendesha shughuli zake peke yake
lakini utaratibu wa mariika huunganisha na kuimarisha kabila zima katika
shughuli zake zote.
Karibu kila mwaka,
maelfu ya wavulana na wasichana wa Gikuyu hutimiza ibada ya tohara, na bila
masharti mengine wakawa katika kundi la hirimu moja (riika rimwe), bila
kujali mbari, muhiriga au wilaya ya kila mtu. Watu hafanya shughuli zao
pamoja kusaidia kabila nao huwa kama ndugu na dada. Hivyo, katika kila kizazi utaratibu wa
kabila la Gikuyu huimarishwa kwa shughuli za hirimu mbali mbali za wazee na
vijana ambao hutenda kwa umoja katika siasa, starehe, dini na uchumi katika
kabila la Gikuyu.
Kutoka kitabu cha Jomo Kenyatta,
Naushangilia Mlima wa Kenya.
|
 |
| Reference |
 |
 |
|
|
 |